Latest News

Sunday, December 7, 2014

Je wajua maana ya kwenda pwani wewe? Ni pwani kweli lakini…kuangalia hapa uwe na umri wa 18+


NAENDA PWANI ni neno la kawaida kwa mtu yoyote anaishi karibu na bahari, lakini neno hilo lina maana nyingine kabisa kwa wakazi wa kijiji cha Bwe juu, huko Mafia Mkoa wa Pwani.  
Mwanakijiji wa Bwe juu akikwambia naenda pwani usidhani kwamba anakwenda kuvua, kuoga, kupunga upepo mwanana wa bahari pamoja na kupoangalia mawimbi makubwa ya bahari, laahasha kuna jambo muhimu sana anakwenda kulifanya akiwa huko pwani.
 
Ukimsikia mtoto, kijana na wazee wanakwambia wanaenda pwani ujue wanaenda kujisaidia haja kubwa, na sio kwenda pwani kama walio wengi wanavyotambua neno hilo la kwenda pwani.  Kama umetoka bara wewe lazima uachwe ukishangaa. 

Wakazi wapata 1000 katika kijiji hicho wanajisaidia haja kubwa katika fukwe nzuri za kijiji hicho, kwa sababu hawana uwezo wa kuchimba vyoo vya kudumu, ambavyo gharama yake ni kubwa sana ukilinganisha na kwenda kujisaidia ufukweni. 
 
“Gharama ya kuchimba choo cha kudumu kwa kutumia matofali ni kubwa sana kwa sababu eneo la kijiji hiki lina mchana mwingi sana, kwa hiyo ukichimba shimo la choo linabomokea mpaka ulijengee kwa matofari, ambayo mpaka uyatoe huko kilindoni”, alisema Hassan Bashiri Mwenyekiti wa kijiji hicho. 
 
Hiyo imesababisha samaki wanaovuliwa katika eneo la kisiwa kidogo cha Bwe Juu, kuwa watamu sana kuliko samaki wanaovuliwa sehemu nyingine tofauti na hapo.  Hassan Bashiri anasema kuwa kijiji hicho kina nyumba zipatazo 150 kati ya hizo nyumba tatu tuu ndio wamechimba choo vya kudumu, nyumba nyingine 147 hawana vyoo na wote wanakwenda kujisaidia katika fukwe za bahari katika kijiji hicho.
Kasimu Hamisi (35) ni mkazi wa kijiji hicho anasema kuwa, hata yeye hajawahi kuchimba choo hata siku moja, yeye na familia yake ya watoto watatu wanakwenda kujisaidia katika fukwe za bahari kila siku. 

“Kila siku mie na mke wangu tunakwenda kujisaidia katika fukwe za bahari tukiamka tuu na jioni, ndio tumezoeya kujisaidia kwenye fukwe toka mie nazaliwa katika kijiji najisaidia kwenye fukwe hadi watoto wangu nao wanajisaidia humo humo.” Alisema Kasimu 

Mohamed Athumani (75), mzaliwa wa kijiji hicho naye pia anakwenda kujisaidia katika fukwe za bahari, anasema kuwa sababu kubwa ya kutochimba vyoo vya kudumu toka kipindi cha ukoroni ni kutokana na  kuwa na mchanga mwingi katika kisiwa hicho na choo ukichimba baada ya siku tatu kinabomokea. 

“Suala la kukosa vyoo kwa wakazi wa kijiji hiki ni cha kawaida tuu, sio hivi sasa tokea kipindi hicho cha ukoloni kulikuwa hakuna vyoo, mpaka sasa watu wanaishi bila ya vyoo na maisha yanakwenda siku hadi siku, tena samaki wa kisiwa hiki kidogo ni watamu sana tena wanatofautiana na samaki wanaovuliwa huko kilindoni kwa sababu ya wanakula kinyesi cha binadamu.” Alisema Mzee Athumani.

Asenga Michael ni mfanyabiashara wa kugandisha samaki wabichi pamoja na kuuza samaki wanaovuliwa kwenye kisiwa hicho, anasema kuwa wateja wengi wanaofika katika duka lake wanataka kuuziwa samaki wanaotoka kisiwa kidogo cha Bwe Juu. 

Mganga Mkuu wa Wilaya ya Mafia, Dokta Credianus Mgimba, anasema kuwa, kuna kesi nyingi sana ya magonjwa ya kuambukiza kama matumbo ya kahara, kuhara damu, homa ya matumbo (Typhoid), hii inatokana na baadhi ya wakazi wa visiwa vidogo kutokuwa na vyoo na kujisaidia kwenye fukwe za bahari. 

“Dawa nyingi tunazoomba kutoka bohari ya madawa ni dawa za magonjwa ya kuhara hii inatokokana na wakazi wengi kujisaidia ovyo katika fukwe pamoja na kuoga katika bahari baada ya kujisaidia,” alisema Mgimba.

No comments:

Post a Comment